Header Ads

Bunge laomboleza Kifo cha Mbunge Profesa Maji Marefu

Spika wa Bunge Job Ndugai ameeleza kusikitishwa na kifo cha Mbunge wa Korogwe Vijijini, Stephen Ngonyani aliyefariki usiku wa kuamkia leo wakati akiendelea kupatiwa matibabu katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, jijini Dar es Salaam.

“Spika wa Bunge Mheshimiwa Job Ndugai anasikitika kutangaza kifo cha Mbunge wa Jimbo la Korogwe Vijijini mkoani Tanga, Mheshimiwa Stephen Ngonyani, maarufu kwa jina la Profesa Maji Marefu, kilichotokea usiku wa leo (jana usiku) 2 Julai, 2018 katika Hospitali ya Taifa Muhimbili,” Bunge limeeleza.

Taarifa ya Bunge iliyosambazwa na Kitengo chake cha Habari, Elimu na Mawasiliano imebainisha kuwa chombo hicho kinaendelea kuratibu mazishi kwa kushirikiana na familia ya marehemu na kuongeza, “taarifa zitaendelea kutolewa.”

Profesa Maji Marefu ambaye alizaliwa 25 Mei, 1952, amekuwa Mbunge wa Jimbo la Korogwe Vijijini tangu mwaka 2010.

Mwaka 2015 alichaguliwa tena kuingia kwenye chombo hicho cha kutunga Sheria lakini katika awamu hii, ameshindwa kushiriki mikutano kadhaa ya Bunge kutokana na kusumbuliwa na ugonjwa ambao umesababisha kifo chake.

No comments:

Powered by Blogger.